Royal Tour imeleta mazao lukuki ya utalii- DK Abbasi

 Na John Mapepele

Katibu Mkuu wa Maliasili na Utalii na Mwenyekiti wa Kamati ya Kuitaingaza Tanzania ya Royal Tour, Dkt. Hassan Abbasi amesema wakati Tanzania imetimiza mwaka mmoja toka Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan atoke ofisini na kucheza filamu ya Royal Tour, kumezaliwa mazao mbalimbali ya utalii hapa nchini.

Dkt. Abbasi ametoa kauli hiyo leo Mei 1, 2023 wakati akihitimisha mjadala wa kitaifa kwenye mtandao (Zoom Meeting) uliojumuisha wadau mbalimbali wa utalii  duniani na  kurushwa mubashara  ya  mitandao na vyombo  mbalimbali vya habari ulioangazia mafanikio  yaliyopatikana  katika kipindi cha mwaka mmoja wa Royal Tour.

Amesema kutokana shuhuda nyingi zilizotolewa na wadau kuwa  kumekuwa na mafanikio makubwa katika kipindi kifupi tangu Roal Tour ilipozinduliwa  inapaswa  kila mtanzania kuwa balozi wa  kuitangaza Tanzania ikiwa ni mkakati wa kuunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya sita ya kutangaza  vivutio vya utalii kwa maslahi ya watanzania na Taifa kwa ujumla.

Pia amemshukuru Mhe. Rais Samia  kwa  maono yake ya kuifungua Tanzania  duniani kupitia Filamu hiyo  na kupongeza  balozi za Tanzania katika mataifa mbalimbali kushiriki kikamilifu katika  kuitangaza vivutio vya utalii.

Amefafanua kuwa Wizara  ya Maliasili na Utalii chini ya Waziri Mohamed Mchengerwa  itaendelea kushirikiana na wadau wote wa utali katika kutangaza  mazao yote ya utalii  badala ya kutegemea  mazao ya awali pekee  ya utalii wa Wanyama.

“Nilipata bahati  ya kushiriki kwenye mkutano wa dunia ambapo  mkutano  ule ulihitimisha kuwa kwa sasa uzoefu  ndiyo  msingi wa  utalii, hivyo basi tutaendelea  kutoka katika dhana  ya kutegemea  utalii wa aina moja na badala yake  kutakwenda mbali zaidi hadi kwenye utalii wa utamaduni kwa kuwa nchi yetu ina hazina kubwa  wa utamaduni”. Amefafanua 

Aidha, ameongeza kuwa   Serikali imeandaa mkakati wa kutengeneza  mabalozi wa  kutangaza utalii wa Tanzania  kwenye  makundi mbalimbali duniani.

Kamishna wa Hifadhi za Taifa (TANAPA) Wiliam  Mwakilema  ametoa ushuhuda  kuwa  filamu ya Royal Tour imeleta matokeo chanya katika eneo la kuongezeka mapato na wageni katika hifadhi zile mbili za Kilimanjaro na Serengeti ambazo Mhe. Rais alipita kucheza  filamu  hiyo.

Kwa upande wake Fatuma Hamis ambaye ni Katibu Mkuu anayeshughulikia sekta ya Utalii Zanzibar amesema  Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano zitaendelea  kushirikiana na wadau wa utalii ili  kuutangaza utalii wa Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Chama cha kuhudumia watalii (TATO) Sirili Akko amefafanua kuwa kutokana na Royal Tour watalii wameanza kurudia safari za kuja nchini huku wakiongeza  siku za kukaa ambapo  pia amesema  filamu imeleta hamasa  kubwa  na kufanya Taasisi za Serikali kuwa karibu  na  vyama  mbnalimbali vya utalii.

Mtendaji Mkuu wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Gilead Teri amesema ujio wa Royal Tour umefanya usajili wa uwekezaji kuwa mara dufu katika kipindi hiki huku kukiwa na ongezeko la mtawanyiko wa uwekezaji katika mikoa  zaidi ya Dar es Salaam na Arusha iliyokuwepo  hapo awali.

Post a Comment

Previous Post Next Post