Na John Mapepele.
Ikiwa imebaki siku moja kuelekea kwenye Tamasha kubwa la aina yake la Utamaduni la Mkoa wa Kilimanjaro litakalofanyika Januari 22,2022 vikundi mbalimbali vya utamaduni kutoka kwenye makabila yote ya mkoa wa Kilimanjaro vimetoa burudani ya kukata na shoka kwa wakazi wa mji wa Moshi na viunga vyake leo Januari 20, 2022 kwenye Uwanja wa Chuo cha Ushirika Moshi, ikiwa ni maandalizi ya mwisho ya tamasha hilo.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mhe, Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi Tamasha hili linaratibiwa na Serikali na Chama cha Machifu nchini ambapo mwenyekiti wa machifu wa makabila yote ya Mkoa wa Kilimanjaro Frank Mareale amewaongoza machifu wenzake wa Mkoa huo huku Serikali ikiwakilishwa na Uongozi wa Mkoa na Wizara yenye dhamana ya utamaduni ikiwakilishwa na Katibu Mkuu Dkt. Hassan Abbasi na Naibu wake Said Yakub.
Baadhi ya Wananchi waliojitokeza wamepongeza jitihada ya Serikali inayoongozwa na Mhe. Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha utaratibu wa kuwa na matamasha ya utamaduni ambayo yatasaidia kuitangaza Tanzania kimataifa na kuliingizi Serikali mapato.
Mratibu wa Machifu wa Mkoa wa Kilimanjaro Joseph Msele ameipongeza Serikali na kufafanua kuwa kinachotokea sasa ni mapinduzi makubwa kwenye sekta ya utamaduni nchini ambapo amesema vikundi mbalimbali vya muziki wa asili na vikundi kwa ajili ya maonesho ya vyakula vya asili vimekamilisha maandalizi yote na vimepania kuionesha dunia urithi wa utamaduni wao .
Ametoa wito kwa wananchi wote kujitokeza kushiriki kwenye tamasha la mkoa wa Kilimanjaro ambalo hilo ambapo amesema milango wa Chuo cha Ushirika Moshi ambapo tamasha hilo litafanyika itakuwa wazi kuanzia saa 12 asubuhi.