Mhe. Gekul atumia Orange Concert kuwakaribisha watu Serengeti, kikundi cha hamasa cha Wizara chaupiga mwingi

 Na. John Mapepele 

Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe Pauline Gekul amewakaribisha wadau mbalimbali kushiriki kwenye tamasha Kubwa la Muziki la Serengeti liliolatibiwa na Wizara yake litakalofanyika jijini Dodoma Machi 12-13,2022 jijini Dodoma.

Wito huo ameutoa wakati wa kilele cha maadhimisho ya siku ya wanawake Duniani  Machi 8, 2022 kwenye Tamasha la aina yake la Orange Concert na harambee ya uchangiaji wa Timu ya Taifa ya  wanawake(Twiga Stars) ambapo zaidi ya  milioni 377 zilichangishwa.  

Tamasha hilo lililoenzi ubunifu wa sekta za sanaa na michezo ambapo taasisi ya wasanii ya Dadahood na Baraza la Michezo Tanzani ziliungana pamoja na mambo mengine kutumia sanaa kuwachangia Twiga Stars.

Katika tamasha hilo mbali na wasanii mbalimbali kutoa burudani za kutosha kikundi cha hamasa cha wizara ya utamaduni, sanaa na michezo kilimetia fora katika mtindo wake wa kutumbuiza ambapo awali kilikaa nje ya ukumbi na kuwakaribisha wageni kwa matarumbeta. 

Kikundi hiki kimeundwa na watumishi na wataalam wa utamaduni na sanaa ambapo kimekuwa  kikitoa hamasa kubwa inayowavutia wengi kwenye shughuli na matamasha  yanayoandaliwa na  Wizara kama mashindano ya soka ya Bara la Afrika kwa wenye ulemavu (CANAF) na mashindano ya Taifa CUP.

Katika tamasha hilo Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alituma ujumbe wa kuchangia milioni 10 kupitia kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo. Baada ya muda Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania naye kupitia kwa Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Mchemba, akapiga simu na kuchangia milioni 15.





Post a Comment

Previous Post Next Post