WANANCHI WAIPONGEZA DAWASA KUMALIZA UKATILI WA KIJINSIA

 WANANCHI wa Mtaa wa Aman, Kata ya Kipunguni wameipongeza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kwa kumaliza tatizo la unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake.

Ni baada ya kukamilisha mradi wa maji Kwa Mkolemba unaowanufaisha zaidi ya wakazi 3,000 wa eneo hilo na kuhitimisha adha ya ukosefu wa huduma. 

Awali, walikuwa wakitumia maji ya kuvuta kwa mkono kutoka visima yalivyokua yanahatarisha afya zao.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wa eneo hilo, Mwenyekiti wa Mtaa wa Amani, Ndugu Daniel Malagashimba ameipongeza Serikali kwa kuwakumbuka wananchi wa mtaa wake ambao waliteseka kwa muda mrefu kwa kukosa huduma hiyo muhimu.

"Nashukuru kwa sasa maji tumeyaona na wananchi wangu wana maji,” amesema Malagashimba na kuongeza:

“Wapo wanawake walionyanyaswa kwa kupigwa na wanaume zao kisa tu walirudi nyumbani bila maji kitendo ambacho ni unyanyasaji wa kijinsia na sasa ukatili huu umemalizika, asanteni sana DAWASA."

Malagashimba anaungwa mkono na Bi. Zainabu Kimei wa mtaa wa Amani ambaye amefurahishwa kwa huduma hiyo kuwafikia kwa mara ya kwanza. 

"Tunashukuru sana maji yamefika Kipunguni, wazee tulikua tunapata tabu kuvuta maji ya kisimani lakini sasa tunafungua tu kwenye bomba,” amesema

“Lakini zaidi kiafya tupo salama kwani maji haya yamepimwa na hayawezi ingia uchafu kirahisi kama tunayovuta toka kisimani ambayo mtu huweza kuyachafua kwa wepesi," amesema Bi Zainabu.

Kwa upande wake, Meneja wa usambazaji maji nje ya mtandao (off grid services), Mhandisi Lilian Masilago amesema DAWASA inafanya juhudi kukamilisha zoezi la kufikisha huduma ya maji katika maeneo yaliyosalia.

"Tunatambua kuna maeneo yamesalia, tunafanya juhudi kubwa kuhakikisha maeneo hayo yanapata huduma,” amesema Mhandisi Lilian

Amesema, “ni imani yangu mtaenda kutunza mradi huu na miundombinu yake ili iweze kuwa na manufaa makubwa kwa wananchi wengi."

Meneja Uhusiano Dawasa Nelly Msuya akiongoza zoezi la ufunguaji maji kama ishara ya kumtua mama ndoo kichwani
Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Amani Kata ya Kipunguni Daniel Malagashimba akimtua mama ndoo kichwani

Post a Comment

Previous Post Next Post