FANYENI KAZI KWA WELEDI NA MAARIFA, KILA MTU ASIMAME KWENYE NAFASI YAKE - LUHEMEJA

 Watumishi wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) wamekumbushwa kuacha uoga na kufanya kazi kwa weledi, maarifa na kulingana na nafasi walizokuwa nazo.

Hayo yamesemwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Dawasa Mhandisi Cyprian Luhemeja katika kikao kilichofanyika na Madereva wa Mamlaka mwishoni mwa wiki.

Akizungumza wakati wa kikao hicho, Afisa Mtendaji Mkuu Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema kada ya udereva ni kada muhimu katika utumishi wa umma hivyo lazima waheshimu kazi yao.

Amesema mkutano huo na madereva unalenga kuzungumza nao masuala mbalimbali ya kimkakati katika kuboresha ufanisi upande wa nafasi za udereva kwani nao ni kada muhimu katika watumishi wa umma na ndiyo watendaji wakuu wa kazi za kila siku.

Mhandisi Luhemeja amewakumbusha watumishi hao kutunza vitendea kazi vyao ambavyo ni Magari huku akiagizia idara ya masuala ya usafiri kutokubadilisha madereva bila idhini yake. 

"Nataka watumishi ninyi kutunza vitendea kazi vya Mamlaka sababu nyie ndio mnayamiliki kwahiyo yawekwe katika hali ya usafi na natoa maagizo hakuna madereva kubadilishwa bila idhini yangu," amesema.

Vile vile , Mhandisi Luhemeja amewakumbusha kufanya ukarabati (service) kwa wakati  ili kutochelewesha shughuli za Mamlaka.

Afisa Mtendaji Mkuu amekuwa na utaratibu wa kukutana na watumishi wa kada tofauti tofauti na kujadili nao masuala mbalimbali na kutatua changamoto ili malengo ya taasisi yaweze kufikiwa.
 
Afisa Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) Mhandisi Cyprian Luhemeja akizungumza na madereva wa Taasisi hiyo wakati wa kikao chake na kuwataka waache uoga na kufanya kazi kwa uweledi.

Post a Comment

Previous Post Next Post