DAWASA YATOA ELIMU YA UHIFADHI WA MAJI KATIKA WIKI YA MAZINGIRA


Mwandishi Wetu,

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) ni miongoni mwa taasisi zinazoshiriki Maadhimisho ya Wiki ya Mazingira Kitaifa yanayoendelea katika Viwanja vya Ukumbi wa Jakaya Kikwete jijini Dodoma, yakiwa na kauli mbiu isemayo: “Dira 2050: Tuwajibike Kukijanisha Tanzania.”

Maadhimisho hayo yanayofanyika kuanzia Juni 1 hadi 5 kila mwaka yamewakutanisha wadau kutoka sekta za umma na binafsi kwa lengo la kuhamasisha uhifadhi wa mazingira, matumizi endelevu ya rasilimali za taifa na kujadili mikakati ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa maadhimisho hayo kitaifa, Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, amesisitiza umuhimu wa utunzaji wa mazingira katika kufanikisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Amesema juhudi za uhifadhi wa mazingira zinapaswa kupewa kipaumbele kupitia upandaji miti kwa kiwango kikubwa, kupunguza uchafuzi wa mazingira, kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi pamoja na kuimarisha biashara ya kaboni na utekelezaji wa miradi ya kijani.

Katika maadhimisho hayo, DAWASA inashiriki kupitia banda la Wizara ya Maji na Taasisi zake, ambapo inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu huduma za majisafi na usafi wa mazingira, umuhimu wa kulinda vyanzo vya maji, pamoja na miradi na mikakati mbalimbali inayotekelezwa na Mamlaka kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji kwa wananchi sambamba na umuhimu wa Wananchi katika kulinda vyanzo vya maji kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.



Post a Comment

Previous Post Next Post