
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhandisi Hamad Yussuf Masauni amesema serikali imeimarisha ushirikiano wa kimataifa na kutoa mchango mkubwa katika masuala ya kikanda na kimataifa yanayohusu mazingira na mabadiliko ya tabianchi.
Masauni ameeleza hayo leo Machi 3, 2026 Unguja, Zanzibar wakati akitoa kauli ya Serikali katika Maadhimisho ya Siku ya Mazingira Afrika inayoadhimishwa siku kama ya leo kila mwaka.

Amesema kupitia ushawishi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika medani ya kimataifa, Tanzania imepata fursa za kuongoza masuala mbalimbali ya kikanda ambayo ni pamoja na kuwa mwenyeji wa Mkutano wa Nishati wa Wakuu wa Nchi za Afrika – Misheni 300 uliofanyika Januari 27 hadi 28 Januari, 2025 jijini Dar es Salaam.
Pia Tanzania ilifanikiwa kuwa mjumbe wa kudumu wa Kamati ya Umoja wa Afrika ya Wakuu wa Nchi na Serikali kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mhandisi Hamad Masauni kuwa Makamu Mwenyekiti wa Mkutano wa Nane wa Baraza la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEA – 8) kuanzia Desemba 2025 hadi Desemba 2027.

Amesema Maendeleo na ukuaji wa taifa lolote duniani pamoja na ustawi wa watu wake vimefungamana na hali na ubora wa mazingira. Hali ya mazingira ikiwa imara ukuaji wa uchumi na ustawi wa watu pia huwa imara.
“Tarehe 3 Machi ya kila mwaka, Bara la Afrika huadhimisha Siku ya Mazingira Afrika, siku hii adhimu iliasisiwa mwaka 2002 na Baraza la Mawaziri la Umoja wa Afrika ikiwa ni moja ya maazimio muhimu ya Umoja wa Afrika katika kuhimiza nchi wanachama na Bara la Afrika kutunza na kuhifadhi mazingira,”
“Kauli mbiu: “Uhakika wa upatikanaji Endelevu wa Maji na Mifumo Salama ya Usafi wa Mazingira ili kufikia Malengo ya Ajenda 2063,” amesema Masauni.

Amesema kwa kutambua uhalisia huu, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa imedhamiria kufungamanisha kwa vitendo masuala ya mazingira, mabadiliko ya tabianchi na maendeleo endelevu.
Ameongeza kuwa Dira 2050 imeweka nguzo adhimu inayohusu uhifadhi wa mazingira na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi. Vile vile, Ilani ya CCM imeweka masuala ya mazingira na mabadiliko ya Tabianchi kama mojawapo ya masuala muhimu yatakayozingatiwa katika kipindi cha mwaka 2025 – 2030.
Masauni amesema dunia inapitia katika changamoto kuu tatu za Mazingira ambazo ni: Upotevu wa Bioanuai; uchafuzi wa Mazingira kutokana na vyanzo mbalimbali pamoja na Mabadiliko ya Tabianchi.
Amesema, uhalisia huu unakumbusha umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kuimarisha uhifadhi wa mazingira pamoja na ufumbuzi wa pamoja wa changamoto za mazingira, ni kwa muktadha huu, Tanzania ni nchi mwanachama wa mikataba mbalimbali inayohusu hifadhi na usimamizi wa mazingira.