SERIKALI YAAHIDI KUBORESHA HUDUMA ZA RADIOGRAFIA

 Na, WAF-Arusha

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko, amesisitiza dhamira ya Serikali ya kuboresha huduma za uchunguzi na mionzi kwa njia ya radiografia nchini ili kuhakikisha huduma zinazotolewa zinaendana na viwango vya kimataifa.

Dkt. Biteko ameyasema hayo leo Oktoba 09, 2024 wakati akifungua Kongamano la Radiografia Afrika lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Arusha (AICC), ambapo amewahakikishia washiriki kuwa Serikali inatambua na kuthamini mchango wao katika sekta ya afya na amewataka kulinda taaluma yao kwa bidii.

“Serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa kwenye miundombinu, vifaa na vifaa tiba, lakini uwepo wa vifaa peke yake hautoshi, tunahitaji wataalamu kama ninyi muweze kuwahudumia Watanzania,” amesema Dkt. Biteko.

Aidha Dkt. Biteko amebainisha kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajia huduma bora kwa wananchi na amewataka radiografia kuhakikisha kuwa wanatoa huduma bora kwa wagonjwa bila kuruhusu vitendo vya rushwa.

Kwa upande wake Naibu Waziri wa Afya Dkt. Godwin Mollel amesema Serikali imenunua PT Scan kwa ajili ya kuangalia saratani ambayo ingedhihirika miaka mitatu (3) na zaidi ambayo ni teknolojia kubwa na kwa nchi za Afrika, Tanzania ni nchi ya nne inayotoa huduma ya  mionzi Tiba.

Pia, Dkt. Mollel amesema uwekezaji uliofanywa na Rais Dkt. Samia umepunguza rufaa kwa asilimia 97 na kuifanya Tanzania kutibu wananchi kutoka nchi jirani kutokana na uwekezaji wa Serikali ndani ya miaka mitatu (3).

“Baada ya uwekezaji huu ambao Rais Samia ameufanya, Tanzania tumeweza kuokoa maisha ya watu ambao hawakuwa na matarajio ya kupona kutokana na magonjwa yanayowakabili, lakini wataalamu wetu wameweza kusoma vifaa hivyo na kutoa huduma sahihi na bora kwa wananchi,”. amesema Dkt. Mollel

Kwa upande wake  Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Paul Makonda amesema Serikali imewekeza zaidi ya bilioni 72 kwa ajili ya kuboresha huduma za afya kama vile kununua dawa, vifaa na vifaa tiba pamoja na kuboresha miundombinu ya afya.





Post a Comment

Previous Post Next Post