Mhe. Mchengerwa awapongeza wadau kupaisha uchumi

Na John Mapepele 

 Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa amewapongeza wadau wa sekta za Sanaa na Burudani kwa kuchangia kwa kiasi kikubwa kwenye uchumi wa taifa.  

Taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2021 imeeleza iliyosomwa na Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Mwigulu Nchemba imeeleza kuwa katika mwaka 2021 eneo la Sanaa na Burudani limechangia kwa asilimia 19.4

“Shughuli za kiuchumi zilikuwa na ukuaji mkubwa katika kipindi cha mwaka 2021 ni pamoja na Sanaa na Burudani (asilimia 19.4)” imefafanua sehemu ya taarifa hiyo.

Katika kipindi cha mwaka 2020 eneo hilo lilichangia asilimia 13.7 hivyo kufanya ongezeko la asilimia 5.7 katika kipindi cha mwaka mmoja tu. 

Wadau mbalimbali wa sekta ya sanaa na burudani wameipongeza Serikali ya awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa mikakati inayobuniwa na Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo ya kuinua na kuboresha sekta hizo katika kipindi kifupi.

“Nimefarijika sana kusikia kuwa sekta zetu za sanaa na burudani sasa zimekuwa na mchango mkubwa.

Ninaamini kuwa hii yote ni kwa sababu ya mageuzi makubwa yanayofanywa na Rais kupitia wasaidizi wake katika Wizara yetu ya Utamaduni na Michezo” amefafanua Msanii nguli nchini Mrisho Mpoto.

Aidha Mhe. Mchengerwa amesisitiza kuwa dhamira ya Serikali kwenye Sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo ni kuhakikisha kuwa wasanii wanaboreshwa, wananufaika na kazi zao na hatimaye wanachangia kwenye uchumi wao na taifa kwa ujumla.

Ameongeza kuwa kwa sasa Wizara imejipanga  kuibua vipaji vingi zaidi nchi nzima kupitia program yake ya kuibua vipaji ya Mtaa kwa Mtaa.

Naye msanii mshindi wa kwanza kwenye mashindano ya sanaa ya muziki wa kizazi kipya ya Taifa Cup 2021 Abisai Kasanga ameipongeza Wizara kwa kuja na mikakati ya Taifa Cup inayoibua vipaji huku akifafanua kuwa hayo ni mageuzi makubwa ambayo yatasaidia kuwapata wasanii wengi wenye vipaji. 

Mara kadhaa Waziri Mchengerwa amesikika akisisitiza kauli ya “vijapi vyako, mtaji wako” kwenye matukio mbalimbali ya wadau wa Sanaa na Michezo  ikiwa na maana  kuwa  vipaji vya sanaa  michezo ni mtaji mkubwa kwa  vijana endapo wakiamua  kuvitumia kikamilifu  ambapo hatimaye vitakwenda kubadilisha maisha yao na uchumi kwa ujumla.

Post a Comment

Previous Post Next Post