BARABARA YA HAYDOM-MBULU KUJENGWA KWA LAMI

   

********************************** 
Na Mwandishi wetu, Mbulu
NAIBU Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Godfrey Kasekenya amewaahidi wananchi wa Wilaya ya Mbulu Mkoani Manyara, kuanzwa kwa ujenzi wa kilomita 50 za barabara ya lami ya Haydom-Mbulu.
Barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 389 imeanzia wilayani Karatu mkoani Arusha, Mbulu- Haydom mkoani Manyara, Sibiti-Lalago mkoani Simiyu, hadi Kolandoto mkoani Shinyanga.
Naibu Waziri Kasekenya amesema barabara hiyo ya lami itaanza kujengwa kilomita 50 kwenye mwaka huu wa fedha unaoishia mwezi Juni mwaka huu.
Amesema wataanza kujenga barabara hiyo ili kutimiza ahadi ya Rais na utekelezaji wa ilani ya uchaguzi wa CCM ambayo imetamka ujenzi wa barabara hiyo.
“Ahadi zilizotolewa na hayati John Magufuli zitaendelea kutekelezwa na Serikali inayoongozwa na Rais wetu Samia Suluhu Hassan hivyo barabara hii nayo itajengwa kama ilivyoahidiwa kwenu,” amesema Kasekenya.
Mkuu wa Wilaya ya Mbulu, Dokta Chelestino Simbalimile Mofuga amemshukuru Naibu Waziri Kasekenya kulia kwa kuwapa ahadi hiyo kwani wananchi wataondokana na kero ya barabara.
Mbunge wa Jimbo la Mbulu Vijijini, Fratei Maasay amesema barabara hiyo inatumika kusafirisha mazao, abiria na wengine kupelekwa hospitali ya rufaa ya Haydom kupata matibabu.
Mbunge wa Jimbo la Mbulu mjini, Paul Isaay ameishukuru Serikali kwa kujenga daraja la mto Magara linalounganisha wilaya za Mbulu na Babati, hivyo ujenzi wa barabara ya lami ya Mbulu-Haydom itachochea maendeleo.

Post a Comment

Previous Post Next Post