MKANDARASI BWAWA LA KIDUNDA ATAHADHARISHWA KUJIANDAA NA MVUA ZA EL NINO

 

Mwandishi Wetu

Mkandarasi anayetekeleza ujenzi wa bwawa la Kidunda ametahadharishwa na uwezekano wa uwepo wa  mvua za El Nino.

Mwenyekiti Bodi ya Maji ya Taifa, Bwn. Suffian Ally ametahadharisha kwa mkandarasi  kampuni ya Sino Hydro Corporation kuzingatia kwa karibu  utabiri wa hali ya hewa katika utekelezaji wa mradi huo. 

Amesema utabiri umeonesha uwezekano wa mvua za El nino kunyesha mwishoni mwa mwaka 2026  hivyo aweke mpango kazi ambao hautaathiriwa na hali hiyo.

Amesema hayo  alipoongozana na wajumbe wa Bodi hiyo kutembelea mradi wa Kidunda unaolenga kupambana na upungufu wa huduma ya maji jijini Dar es salaam na maeneo jirani. 

Amesema maendeleo ya mradi huo yanaridhisha lakini ujenzi haupaswi kusimama kwa kisingizio cha mvua bali kufanya maandalizi mapema ili kukabiliana na hali hiyo.

Naye Katibu wa Bodi hiyo ambaye pia ni Mkurugenzi Rasilimali za Maji Wizara ya Maji, Bwn. Robert Sunday amempongeza Rais wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kusimamia vizuri mapato ya ndani ambayo yamewezesha kutekelezwa kwa mradi huo. Amesema wazo la ujenzi wa mradi huo lilianza zaidi ya mika 50 iliyopita hadi Rais Dkt. Samia alipoamua kulitekeleza kwa kutumia fedha za ndani. 

Amesema ni uthubutu ambao unapaswa kupongezwa na kila Mtanzania na  kuwahakikishia Watanzania kuwa mradi huo utakamilika na kuimarisha huduma ya maji kwa wananchi wa Jiji la Dar es Salaam na maeneo jirani.

Kwa upande wake Mwenyekiti Bodi ya Maji Bonde la Wami Ruvu Nickson Lutenda amesema vyanzo vyote vya maji vinavyotiririsha maji katika bwawa hilo vitaendelea kulindwa ili kuwezesha uendelevu wa bwawa nakusisitiza  wananchi wajiandae kuchangamkia fursa zinazotokana na bwawa hilo ikiwemo kilimo na ufugaji.

Bwawa la Kidunda linatekelezwa kwa fedha za ndani zaidi ya shillingi bilioni 300. Ujenzi wake umefika asilimia 52.4


Post a Comment

Previous Post Next Post