Mwandishi Wetu,
Mradi wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi utekelezaji wake umefika wastani wa asilimia 72, ambapo kikao kimefanyika kuhusu maendeleo yake.
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji Bi Rose Ambrose ameongoza kikao kazi kujadili maendeleo ya mradi huo unaofadhiliwa na serikali ya Ujerumani, GCF ( Green Climate Fund) kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania
Mratibu wa mradi huo Mhandisi Annastazia Bulogo amesema, "Mradi umefikia asilimia 71.8 na unatarajiwa kugharimu kiasi cha Shillingi Bilioni 440 za Tanzania mpaka kukamilika kwake na unatarajiwa kukamilika ifikapo Agosti, 2027
Naibu Katibu Mkuu, Bi Rose Ambrose, amekihakikishia kikao kuwa Wizara inajitahidi katika hali zote kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati, licha ya changamoto kadhaa zinazotafutiwa majibu.
Amewaahidi wajumbe wa kikao kuwa, changamoto zote zilizojitokeza na zitakazojitokeza, Wizara itazitatua kwa wakati kuhakikisha Mradi unakamilika kwa wakati.
Amemtaka Msimamizi wa Mradi huo Mhandisi Annastazia Bulogo kukutana na wadau kutoka Wizara za kisekta ili kuona namna bora ya kuondosha changamoto.
Kikao kimehudhuriwa na wawakilishi kutoka wizara za Fedha, TAMISEMI, Kilimo, Afya, Uvuvi na kinatarajiwa kufanyika tena mwezi Agosti 2026.


