
WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Dk. Ashatu Kijaji, amezindua Bodi ya tano ya ushauri ya Wizara kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) hii leo Februari 13, 2026 Jijini Dodoma.
Bodi hiyo imeelekezwa kubuni mikakati thabiti ya kukuza uchumi wa viwanda kupitia rasilimali za misitu na nyuki kwa kushirikiana na wananchi na sekta binafsi, sambamba na kusimamia maelekezo ya Kamati ya Mawaziri nane kuhusu kutatua migogoro ya maeneo ya hifadhi yaliyovamiwa.

Dk. Kijaji pia ameipongeza TFS kwa kutatua migogoro 423 kati ya 438 (asilimia 96) na kuitaka kuendelea na kazi hiyo kwa uzalendo na utu, ili kujenga imani ya wananchi na kuendeleza ulinzi wa maliasili kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho.
Aidha, Waziri ameielekeza bodi hiyo kuimarisha utalii wa ikolojia na malikale, pamoja na kuboresha miundombinu ya vivutio vya utalii kuvutia watalii wengi zaidi na kuongeza pato la taifa, kwa lengo la kufikia watalii milioni 8 ifikapo mwaka 2030.