SERIKALI YAWAVUTIA KASI WATUMISHI WAZEMBE

Na Lusungu Helela- Tabora

 Serikali imesema haitawavumilia Watumishi wa Umma  wenye kasumba ya kufanya kazi kwa mazoea hali inayopelekea malalamiko kutoka kwa wananchi kwa  kushindwa kupata huduma bora 

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Deus Sangu ametoa kauli hiyo leo wakati akizungumza kwenye Kikao kazi cha  Watumishi wa Manispaa ya Tabora  mara baada kusikiliza changamoto zinazowakabili na kuzitafutia ufumbuzi, ikiwa ni ziara ya kimkakati ya kuwafuata watumishi katika maeneo yao ya kazi  badala ya kuja Dodoma

Amesema tabia hiyo imekuwa ikikwamisha azma ya Rais  Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan ya kuona Wananchi wanahudumiwa ipasavyo katika ofisi za Serikali

Amewataka Watumishi hao  kutambua kuwa suala la  kutoa huduma bora kwa wananchi si hisani bali ni wajibu 

Katika hatua nyingine Mhe. Sangu amezitaka Mamlaka za ajira na nidhamu kusimamia haki na stahiki zote za watumishi huku akizionya Mamlaka hizo kushauri ipasavyo bila kuwaumiza watumishi kwa lengo la kuwafurahisha Viongozi wao.

Amesema ni jambo la aibu kuona Watumishi  wakiwasilisha changamoto zao  mbele ya Viongozi wa Kitaifa wanapofanya ziara katika maeneo yao  ilhali changamoto hizo zingetafutiwa ufumbuzi katika ngazi ya  Wilaya au Mkoa 

Amesema kitendo hicho  kinaonesha kuwa  baadhi  ya  Watumishi hawawajibiki ipasavyo katika kutekeleza majukumu yao.

 " Haipendezi kuona Watumishi wakiwa hawatimizi wajibu wao wakitumia simu na kupiga soga muda wote kipindi cha muda wa kazi " amesema Mhe.Sangu

Sambamba na hilo Mhe.Sangu ametoa rai kwa Watumishi kujiepusha kutenda vitendo vitakavyopelekea kufukuzwa kazi huku akisisitiza kuwa mchakato  kurudishwa kwenye utumishi wa umma ni jambo gumu

Hivyo, Mhe.Sangu  amewasihi  Watumishi wa Umma nchini  kujiepusha vitendo hivyo  kwani mchakato wake wa kupata kibali cha kurudishwa unachukua muda mrefu.




Post a Comment

Previous Post Next Post