BRELA, WADAU KUADHIMISHA SIKU YA MILIKI UBUNIFU DUNIANI





 Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) Godfrey Nyaisa, amesema Serikali itaendelea kutatua changamoto za matumizi ya Haki Miliki ili kuwawezesha Wajasiriamali na wabunifu nchini kukuza Biashara na kulinda Bunifu zao.

Nyaisa ametoa kauli hiyo kwenye mkutano na waandishi wa Habari Jijini Dar es salaam katika kuelekea maadhimisho ya Miliki Bunifu Duniani inayoadhimishwa April 26 kila mwaka ambapo kwa kwa mwaka huu Tanzania itaadhimisha siku ya April 28 katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha (Julius Nyerere International Convention Center -JNICC).

“Maadhimisho haya yana lengo la kutambua mchango wa Miliki Ubunifu hususan Hataza, Hakimiliki, na Alama za Biashara na Huduma” amesema Nyaisa.

Amesema ni wazi kuwa sekta ya Miliki Bunifu imesaidia watanzania wengi kujiajiri hivyo Serikali imekusudia kuleta ujumuishi katika sekta hiyo kwa maslahi ya mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Katika maadhimisho hayo Waziri mwenye dhamana ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dkt Ashatu Kijaji anatarajia kuwatunuku vyeti wabunifu na wajasariamali hao lengo ni kutambua mchango wao.

Kauli mbiu ya Siku ya Miliki Ubunifu kwa Mwaka huu ni, “Wanawake na Miliki Ubunifu: kuongeza kasi ya Ubunifu katika Biashara” lengo la Kauli Mbiu hii ni kutambua mchango wa Wabunifu wanawake katika kukuza Biashara na nafasi yao katika ukuaji wa uchumi nchini.

Tangu kuanza kwa maadhimisho hayo mwaka 2000 watu wamekuwa wakijifunza kuhusu sheria zinazosimamia masuala ya Miliki Ubunifu pamoja na matokeo katika maisha ya kila siku.

Post a Comment

Previous Post Next Post