RAIS SAMIA AIPONGEZA WIZARA YA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO KWA UBUNIFU


Na John Mapepele

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mhe, Samia Suluhu ameipongeza Wizara ya utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kazi kubwa inayofanya ya kuitangaza Tanzania duniani kupitia sekta za Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mhe. Samia ametoa kauli hiyo wakati akipokea Kombe la Dunia la FIFA leo Mei 31, 2022 Ikulu jijini Dares Salaam kutoka kwa kiongozi kikosi cha ziara ya kombe hilo hapa nchini na mchezaji nguli wa Brazil Juliano Belletti.

Amesema Wizara hiyo imekuwa ikifanya ubunifu mkubwa wa kuitangaza Tanzania ambapo katika siku za hivi karibuni kwa kushirikiana na wadau waliandaa tukio la kutazama mbashara fainali za UEFA kupitia DSTv kwenye Daraja jipya la Tanzanite lililopo jijini Dar es Salaam hivyo kuifanya dunia kuendelea kuilifahamu daraja hilo la kisasa na Tanzania kwa ujumla wake.   

"Lakini kutumia lile daraja na wakaonyesha na tukaonekana ulimwengu mzima ile ni jitihada  kubwa, na wameonesha kwamba  Tanzania  tuna vivutio vinavyoweza kutumika na ni ubunifu mkubwa” amesisitiza Mhe. Rais Samia.

Pia, Mhe. Rais amepongeza kwa kuendelea kufanya vizuri kwenye mashindano  mbalimbali ya mpira wa miguu na kufafanua kuwa  yameendelea kuitangaza Tanzania duniani.
Aidha, alitaka ujio wa kombe la dunia utumike  ari kubwa zaidi  kwa timu za taifa  za wanawake  kuendelea kufanya  vizuri zaidi  ili ziweze kufika kwenye mashindano ya dunia  hatimaye kuitangaza Tanzania na vivutio vyake.

Kuhusu kuratibu mkutano mkuu wa  mashindano ya soka ya Kombe la shirikisho la Bara la Afrika (CAF) Mhe. Rais na amesisistiza kutumia vizuri nafasi  hizi  kutangaza  vivutio mbalimbali vya Tanzania na hatimaye kuinua  uchumi wa nchi yetu.

Akimkaribisha kutoa hotuba, Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe Mohamed Mchengerwa amemshukuru Mhe. Rais kwa kuunda wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo na kuendelea kumwamini na kumteua kuongoza Wizara hiyo muhimu ambayo ni nguvu shawishi ya nchi ambapo amesisitiza kuwa wizara yake itaendelea kuwa bunifu zaidi.

Amesema kupitia michezo Tanzania imepata heshima kubwa ambapo amesema kwa sasa Serikali inatekeleza programu ya kuibua  vipaji  wanamichezo na wasanii ya mtaa kwa mtaa,  ujenzi wa shule za michezo,kujenga  viwanja vya kisasa vya ndani kwenye miji  ya Dar es salaam na Dodoma na sasa  kuhakikisha timu za taifa ili ziweze kufanya  vizuri  kwenye mashindano ya kimataifa  ikiwa ni pamoja na timu ya taifa ya wanawake chini ya umri wa miaka 17 ya Serengeti Girls  ili ifuzu kuingia kombe la dunia.

Amesema kinachopaswa kufanya sasa ili kuleta mapinduzi kwenye michezo ni kila mtu kutekeleza wajibu wake  huku akinukuu kauli ya baba wa taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere aliyoitoa  mwaka 1978 ambayo alisema” Inawezekana  endapo  kila mmoja  wetu  akitimiza wajibu wake”

 

Post a Comment

Previous Post Next Post