Mhe. Mchengerwa atoa maneno mazito kwa wachezaji wa Simba masaa machache kabla ya kucheza na Orlando leo

 


Na. John Mapepele

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa leo Aprili  24, 2022 amezungumza na wachezaji wa Timu ya Simba  masaa machache kabla ya kuingia kwenye mechi ya  marudiano na Orlando Pirates katika mashindano ya kombe la Shirikisho barani Afrika na kuwatakia kila la heri katika mchezo huo kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mhe, Samia Suluhu Hassan.

Mhe. Mchengerwa ameongea na wachezaji wa Simba kupitia simu ya Balozi wa Tanzania nchini Afrika Kusini ambapo ametaka  wachezaji kucheza  kwa moyo huku wakitambua kuwa ushindi wa Simba  leo  utaiweka Tanzania  katika ramani ya Afrika ya nchi zenye vilabu vinavyofanya vizuri. 

Aidha, ameongeza kuwa  watanzania  na Serikali ipo bega kwa bega na timu hiyo na kwamba wazingatie zaidi mchezo na wapuuze baadhi ya maneno  kuhusu mambo ya usalama kwakuwa  watanzania na waafrika kusini ni ndugu na marafiki na mchezo siyo uadui.

" Mheshimiwa Rais anamatarajio makubwa sana na mchezo wa leo kwani ni dhamira yake kiuona nchi yetu inafanya vizuri katika mashindano mbalimbali ya kimataifa" amesisitiza Mhe. Mchengerwa

Amesema kwa sasa  akili  na masikio ya watanzania yapo nchini Afrika Kusini na    amewataka wachezaji  na watanzania wote kumtanguliza Mwenyezi Mungu mbele katika mchezo wa leo ili tuweze kushinda.

Timu ya Simba  inatarajia kushuka dimbani kucheza na Orlando Pirates ya Afrika ya Kusini majira ya saa moja usiku kwa saa za Tanzania.

Katika mchezo wa kwanza wa robo fainali Simba iliishinda Orlando 1-0 katika uwanja wa Benjamini Mkapa  Aprili 17, 2022 kwa mkwaju wa penati.

Post a Comment

Previous Post Next Post