SHOLO MWAMBA KUSIMAMISHA DUNIA DUBAI EXPRO LEO, KESHO

 Na. John Mapepele

Mfalme wa muziki wa Singeli nchini, Sholo Mwamba pamoja na msanii wa kizazi kipya Saraphina leo Februari 22, 2022 wanatarajia kupanda   na kuionyesha dunia miziki kutoka Tanzania kwenye onesho kubwa duniani la Dubai Expro. 

Kwa mujibu wa ratiba ya waandaji wa onesho hilo Sholo  Mwamba  ndiye anayeanza kupanda  majira ya saa 9:30 alasiri  na Saraphina anapanda  majira ya saa 10:30 jioni ambapo wote watapanda kwenye ukumbi wa Sea Stage.

Akizungumza kutoka Dubai, muda mfupi kabla ya kupanda jukwaani Sholo Mwamba amesema atahakikisha kupitia shoo ambazo anazozifanya, Singeli inakwenda kuwepo kwenye sura ya dunia.

Ameongeza kuwa muziki wa Singeli una nafasi kubwa ya kuitambulisha Tanzania na kuvutia watalii wengi kuja kutembelea, hivyo atahakikisha wageni watakaohudhuria onesho hilo wanavutiwa  na muziki huo. 

Sholo amepangiwa kutumbuiza mara tatu kwenye onesho hilo leo, kesho Februari 23, majira ya saa 10: 30 jioni wakati onesho lake la mwisho litakuwa Februari 24, 2022 majira ya saa 2:00 usiku.

Kwa upande wa Saraphina pia amepewa nafasi tatu za kutumbuiza kwenye onesho hilo, leo saa 10:30 na saa 2:00 usiku na Februari 26,2022 majira ya saa 1:30 usiku kwenye ukumbi wa Sea Stage. 

Wasanii hao wanatarajiwa kutumia nafasi hiyo kuitangaza Tanzania ikiwa ni pamoja kukiuza kiswahili duniani. 

Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo. Mhe, Mohamed Mchengerwa amefafanua kuwa Tanzania imebarikiwa kuwa na hazina kubwa ya Utamaduni ambao kama utatangazwa vizuri kwenye tamasha hilo utavutia wageni wengi kuja nchini kama watalii hivyo kuliingizia taifa mapato.

Akizungumzia kuhusu maonesho ya wasanii hao, Katibu Mkuu wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. Dkt, Hassan Abbasi amesema ameridhishwa na maandalizi yanavyofanyika na anaamini wasanii hao wataitangaza vema nchi yetu.




Post a Comment

Previous Post Next Post