SERIKALI YAANDAA MKAKATI WA KITAIFA KUKABILIANA NA WANYAMAPORI WAKALI NA WAHARIBIFU

 Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) akijibu swali la Mbunge wa Mikumi ,Mhe. Dennis Londo lililohoji kuhusu mpango wa serikali wa kuhakikisha usalama wa wananchi wanaoishi kwenye vijiji vinavyopakana na hifadhi dhidi ya wanyamapori waharibifu bungeni jijini Dodoma leo.

***********************

Serikali imeandaa mpango mkakati wa Kitaifa wa kukabiliana na wanyama wakali na waharibifu wanaovamia makazi ya watu.

Hayo yamesemwa leo bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Mikumi ,Mhe. Dennis Londo lililohoji kuhusu mpango wa serikali wa kuhakikisha usalama wa wananchi wanaoishi kwenye vijiji vinavyopakana na hifadhi dhidi ya wanyamapori waharibifu.

Mhe. Mary Masanja amesema kuwa mkakati huo unatoa mwongozo wa namna nzuri ya kuwawezesha wananchi kutumia maeneo yao bila kuathiriwa na uwepo wa wanyamapori.

Ametaja moja ya mpango uliowekwa na Serikali ni kutoa mafunzo ya mbinu bora za kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu kwa wananchi wanaoishi katika maeneo ya pembezoni mwa hifadhi nchini kote.

Mhe. Mary Masanja ameongeza kuwa mpango mwingine wa Serikali ni kuimarisha vikosi vya doria za kudhibiti wanyamapori na kuongeza vitendea kazi.

Pia, Mhe. Mary Masanja amefafanua kuwa Serikali itashirikiana na Halmashauri za Wilaya na Vijiji katika kuandaa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi.

Aidha, Mhe. Mary Masanja amesema Serikali imeunda kikosi kazi maalum kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu katika maeneo yanayozunguka hifadhi.

Mhe. Mary Masanja ametoa rai kwa wananchi wa Mikumi na wanaoishi kwenye maeneo mengine yanayozunguka hifadhi kuendelea kutoa ushirikiano na kufuata maelekezo ya wataalam wa wanyamapori kwa kutekeleza mbinu mbalimbali zinazotumika kukabiliana na wanyamapori hao ili kupunguza athari zinazoweza kujitokeza.

Serikali ili kukabiliana na changamoto ya wanyamapori waharibifu itatoa mafunzo kwa wananchi wanaoishi pembezoni mwa hifadhi kuhusu mbinu bora za kukabiliana na wanyamapori wakali na waharibifu,

tutaimarisha vikosi vya doria za kudhibiti wanyamapori na tutashirikiana na Halmashauri za Wilaya na vijiji ili kuwezesha uandaaji wa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi.

Post a Comment

Previous Post Next Post