Mwandishi Wetu,
Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro imeanza utekelezaji wa mpango maalum wa kuboresha eneo la Endoro ili litumike kama sehemu ya utalii tiba kwa watalii pamoja na shughuli nyingine zinazohitaji utulivu.
Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro Abdul-Razaq Badru akiwa na Wakurugenzi wa Bodi katika eneo hilo lenye Maporomoko ya Maji (Water Falls), Mapango ya Tembo, Msitu, Wanyama wakubwa na maarufu kwa utalii wa kutembea (Walking Safaris)
ameeleza kuwa kupitia fedha za Mfuko wa Maendeleo ya Utalii (TDL) eneo la Endoro linaboreshwa kwa ujenzi wa miundombinu ya kisasa ya Utalii ili yatumike kama sehemu za utalii tiba, utafiti, utalii wa kutembea, mapumziko binafsi na kuondoa msongo wa mawazo.
“Endoro ni eneo lenye utulivu, lina kivutio cha Mapango ya Tembo na maporomoko ya maji yenye urefu wa mita 40, mamlaka imeamua kuboresha miundombinu yake ili mgeni akifika hapa na hasira aweze kupata utulivu na kurudi katika hali yake ya kawaida”,alisema kamishna Badru.
Makamu Mwenyekiti wa bodi hiyo Dkt. Harieth Mtae amepongeza jitihada hizo na kusema zitatoa fursa ya kuongezeka kwa idadi ya watalii wanaotembelea kivutio hicho kilichopo hifadhi ya Ngorongoro.
Wakurugenzi wa bodi hiyo pia wamekagua geti la kisasa la kuingilia ndani ya hifadhi linalofanya kazi katika mfumo wa kisasa pamoja na minara ya mawasiliano ndani ya hifadhi inayolenga kuboresha huduma kwa watalii.












