Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Mhe Albert Msando, ameongoza ziara maalum ya viongozi wa Manispaa ya Ubungo katika chanzo cha uzalishaji maji Ruvu Juu kwa lengo la kujionea hali ya uzalishaji na usambazaji wa maji pamoja na kutafuta suluhu ya pamoja ya changamoto za huduma ya Maji.
Ziara hiyo imewahusisha Madiwani wa Manispaa ya Ubungo, viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Ubungo pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama, ikiwa ni sehemu ya juhudi za Serikali za kufuatilia na kuboresha huduma ya maji kwa wananchi.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe Msando amewataka madiwani kushiriki kikamilifu ili kubaini changamoto za maji katika kata zao na kupata uelewa wa kina kuhusu hatua zinazochukuliwa na DAWASA kuboresha huduma hiyo.
Aidha, ameielekeza DAWASA kutoa maelezo kuhusu mipango ya muda mfupi na muda mrefu ya kuimarisha upatikanaji wa maji katika Wilaya ya Ubungo pamoja na kuwapa wananchi taarifa sahihi kuhusu hali ya huduma katika maeneo yao.
Kwa upande wake, Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA, Mhandisi Mkama Bwire, amesema ziara hiyo itasaidia viongozi kupata taswira halisi ya uzalishaji wa maji, mfumo wa usambazaji na mikakati inayotekelezwa kuboresha huduma kwa wakazi wa Ubungo.
Mhandisi Bwire ameeleza kuwa DAWASA inaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuongeza uwezo wa uzalishaji na usambazaji wa maji, ikiwemo ufungaji wa pampu mpya katika mitambo ya uzalishaji.
“Mpaka sasa pampu sita kati ya nane zilizopangwa zimewasili nchini zimewasili, huku pampu mbili zilizobaki zikiendelea kukamilishwa kabla ya kuletwa. Tayari zoezi la ufungaji limeanza na pampu moja imefungwa, huku kazi ikiendelea kwa pampu nyingine,” amesema Mhandisi Bwire.
Ameongeza kuwa maboresho hayo yanatarajiwa kuongeza ufanisi wa uzalishaji na usambazaji wa maji, hatua itakayosaidia kupunguza changamoto za upatikanaji wa huduma katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Ubungo.





