SERIKALI YAENDELEA NA JITIHADA ZA KUKABILIANA NA TEMBO

 Na Mwandishi Wetu,

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan amesema Serikali imeendelea na mikakati mbalimbali ya kukabiliana na wanyamapori tembo katika Halmashauri za Wilaya ya Namtumbo na Tunduru Mkoani Ruvuma lengo ikiwa ni kuzuia wasiingie kwenye makazi ya watu.

Ameyasema hayo leo Septemba 26, 2024 alipokuwa akizungumza na wananchi katika uwanja wa CCM Tunduru Mkoani Ruvuma.

“Kwa upande wa wanyama tembo Serikali tumeanza kuchukua hatua, kwanza tumeweza kuongeza askari ambao wako katika maeneo mbalimbali lakini pia kuna askari wa vijiji wanaosaidiana na askari hawa kuhakikisha tembo hawaingii kwenye makazi ya watu” amesisitiza Rais Samia.

Ameongeza kuwa Serikali imeweka magari ya doria katika Wilaya ya Namtumbo na Tunduru na yanafanya kazi kubwa ya kukabiliana na tembo.

Aidha, amesema Serikali imeweka ndege nyuki “drones” kwa ajili ya kufukuza makundi ya tembo ikiwa ni hatua za awali lakini Serikali itaendelea na jitihada nyingine za kukabiliana na tembo, lengo ikiwa  ni kuongeza idadi ya ndege nyuki na kuimarisha vituo vya askari wa Jeshi la Uhifadhi.






Post a Comment

Previous Post Next Post