TBS IMETOA LESENI NA VYETI 167 KWA WAZALISHAJI AMBAO BIDHAA ZAO ZIMETHIBITISHWA UBORA

     Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Bw.David Ndibalema akikabidhi leseni na vyeti kwa wazalishaji ambao bidhaa zao zimethibitishwa ubora baada ya kukidhi matakwa ya Viwango kwa kipindi cha kuanzia Mwezi Aprili hadi Juni mwaka huu.

Baadhi ya wazalishaji ambao bidhaa zao zimethibitishwa ubora baada ya kukidhi matakwa ya Viwango kwa kipindi cha kuanzia Mwezi Aprili hadi Juni mwaka huu.

**********************************

NA EMMANUEL MBATILO

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limetoa leseni na vyeti 167 kwa wazalishaji ambao bidhaa zao zimethibitishwa ubora baada ya kukidhi matakwa ya Viwango kwa kipindi cha kuanzia Mwezi Aprili hadi Juni mwaka huu.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika Makao Makuu ya Shirika hilo Jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Bw.David Ndibalema amesema Vyeti na leseni hizo ni za bidhaa za vyakula,Vipodozi, Vifaa vya Ujenzi,Vilainishi,Vitakasa Mikono,Vifaa vya Umeme, Vifaa vya Makenika, magodolo, Vibebea pamoja na Vifungashio.

Aidha Bw.Ndibalema amewishukuru Serikali kwa kuwahudumia wajasiriamali wadogo kupitia huduma za TBS juu ya udhibiti ubora bila malipo ya gharama za ukaguzi na upimaji.

“Wajasiriamali hawa wataendelea kuhudumiwa bure kwa kipindi cha miaka mitatu ya mwanzo.Hata baada ya miaka mitatu kuisha,TBS itafanya tathimini ya uwezo wa wajasiriamali ili kupima uwezo wao wa kulipa”. Amesema Bw.Ndibalema.

Hata hivyo Bw.Ndibalema amewahasa wazalishaji hao waendelee kuzalisha bidhaa zinazokidhi matakwa ya viwango kwa mustakabali wa afya na mazingira ya watumiaji kwa ujumla.

Kwa upande wake mfanyabiashara wa kampuni ya Woiso Original Products, wanaoshughulika na utengenezaji wa viatu Bw.Joachim Komba amesema kampuni yao inajivunia kupata cheti kutoka TBS kwani itatanua wigo kwa wateja wao kuwaamini na kutumia kitu ama bidhaa yenye ubora wa hali ya juu.

Vilevile nae Afisa Masoko wa kiwanda cha Yehehe Investment Limited Bw.Godlisen Mwanjala amesema mteja anapohudumiwa na wafanyabiashara anatakiwa akiridhishe kwa kuoneshwa leseni ili kujihakikishia bidhaa hiyo anayonunua imekidhi viwango na inafaa kwa matumizi.

Post a Comment

Previous Post Next Post